KOCHA wa Yanga, George Lwandamina amelazimika kusafiri na beki wake mpya, Fiston Kayembe lakini mazoezi ya siku mbili wakiwa Njombe yakamaliza ubishi kwamba beki huyo anatakiwa kupewa mkataba haraka.
Fiston ambaye alitua wiki iliyopita kwa majaribio mafupi ameonyesha uwezo mkubwa katika mazoezi hayo ambapo ameonekana akiwadhibiti vyema kwa akili washambuliaji tofauti.
Beki huyo raia wa DRC Congo amekubalika kwa uwezo wake wa kukaba kwa nguvu akitumia akili zake huku akiwa mwepesi kuanzisha mashambulizi kwa kupiga pasi za maana.
Kilichomvutia zaidi Lwandamina ni akili ya kuanzisha mashambulizi, uwezo ambao ni mabeki wachache wanaojaliwa kuwa nao, huku kwa Yanga akiwa nao Kevin Yondani pekee.
Tayari Lwandamina ameshawapa mkono wa Baraka mabosi wa klabu hiyo chini ya mwenyekiti wa kamati ya usajili Hussein Nyika kuendelea na kazi ya kumsainisha mkataba beki huyo.