STAA wa Bongomuvi, China Zahor ameponea chupuchupu kwenye ajali mbaya ya pikipiki iliyomtokea Jumatano maeneo ya Gerezani, jijini Dar es Salaam, katika makutano ya barabara ya Kilwa na ile iendayo Stesheni.
Akiongea na Saluti5, China amesema kuwa akiwa anatokea Posta kuelekea nyumbani kwake Mtoni Mtongani, gari ndogo ilikuja kasi na kumzoa kwa nyuma na kusababisha arushwe kando na pikipiki yake kuharibika vibaya.
“Hali yangu ndio kama unavyoniona, nimeumia sana sehehu za kichwani ambapo nimeshonwa nyuzi 13 ambapo hata hivyo hivi sasa ninaendelea vyema wakati jitihada za kumsaka dereva aliyesababisha ajali zikiendelea,” amesema.