KILA Alhamisi kuanzia wiki ijayo, wakongwe wa muziki wa dansi, Msondo Ngoma Music Band watapatikana ndani ya Equator Grill, Mtoni kwa Azizi Ally jijini Dar es Salaam, imefahamika.
Bosi wa Equator Grill, Hamis Slim ameitonya saluti5 kuwa shoo ya Msondo Ngoma ndani ya ukumbi huo itakuwa ikidondoshwa kuanzia mishale ya saa 1:00 jioni, huku kiingilio kikiwa ni ustaarabu wako tu.
“Hii ni fursa nyingine tena kwa wakazi wa Mtoni na maeneo jirani kupata raha za wana Msondo Ngoma kila wiki katika siku za Alhamisi, ambapo vibao vyao vipya na vya zamani vitakuwa vikikung’utwa,” amesema Slim.
Kabla ya awamu hii kuibuka tena ndani ya ukumbi huu, wakongwe hao waliwahi kuwa wanatumbuiza hapo lakini ikiwa ni kwa siku za Jumatano na kwa kiingilio cha sh. 3,000 ambapo baadae waliamua kusitisha kwa sababu zisizojulikana.