WAIMBAJI Juma Katundu na Abdallah Hemba wametupia kwenye mtandao wa kijamii picha waliyopiga pamoja na kuipa maneno mengi chini yake wakisisitiza kuwa wao watabaki kuwa ndugu wanaotoka mkoa mmoja wa Pwani, licha ya kuwa kwenye bendi mbili tofauti zenye upinzani mkali.
Hemba ni kiongozi ndani ya bendi kongwe ya muziki wa dansi ya Mlimani Park “Sikinde Ngoma ya Ukae”, alkadhalika katundu nae ni kiongozi katika Msondo Ngoma Music Band.
Kwenye picha hiyo ambayo wanaonekana wameketi kindugu zaidi wakifurahia maisha, wawili hao wameandika; “Sisi tutabaki kuwa ndugu na upinzani wetu utaishia jukwaani tu!”
Katika hali ya kawaida ya kimuziki, Katundu na Hemba wamekuwa wakionyesha uhasama mkubwa wa kimuziki unaoshinikizwa na bendi zao, kiasi hata baadhi ya mashabiki kuamini kuwa si watu wa kuweza kukaa pamoja na kupanga maisha kama walivyopambanua katika posti yao.
Kadhalika, Hemba na Katundu wanatofautiana pia hata kwa upande wa ushabiki wa soka la Bongo, ambapo Katundu ni mnazi wa Wekundu wa Msimbazi na Hemba ni mkereketwa wa watoto wa Jangwani.