MOTO mkubwa wa burudani unatarajiwa kuwaka Aprili 28, mwaka huu pale bendi mbili za mipasho za Jahazi Modern Taarab na Tanzania One Theatre (TOT), zitakapotumbuiza jukwaa moja.
Burudani hiyo inayotazamiwa kuwa ya kukata na shoka kutokana na bendi zote hizo kuwa na mashabiki wengi, imepangwa kurindima ndani ya ukumbi wa CCM Mwinjuma, Mwananyamala, jijini Dar es Salaam.
Taarifa kutoka ndani ya bendi hizo inasema kuwa, Mfalme wa Kibao Kata anayetikisa jiji la Dar es Salaam na maeneo jirani hivi sasa, Kivurande Junior, amealikwa kupamba burudani hiyo itakayoanza kuunguruma majira ya saa 3:30 na kuendelea hadi majogoo.
“Tunawaomba mashabiki wote wa mipasho wa maeneo ya Mwananyamala pamoja na Wilaya nzima ya Kinondoni, kuhuduria kwa wingi shoo hiyo ili kufaidi mambo mengi matamu tuliyowaandalia,” ilisema taarifa hiyo.
Hii ni mara ya pili kwa bendi hizo kutumbuiza pamoja ndani ya ukumbi huo, ambapo mara ya kwanza ilikuwa ni mwezi uliopita walipotiririsha burudani kabambe na kukosha nyoyo za mashabiki wote waliohudhuria.